2/10/2016

Mazungumzo ni bora kuliko uchaguzi kurudiwa Zanzibar

               
Mwaka 2015 ulikuwa mwaka wa kihistoria katika jamhuri ya muungano wa Tanzania, yaani kwa kuwa na matukio makubwa, tukio la kwanza ni uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba 25,2015.Nauhita mwaka wa kihistoria kutokana na kampeni za uchaguzi pamoja na uchaguzi wenye kuwa na tofauti na miaka mingine iliyopita toka nchi ipate uhuru.Utofauti huo ni ushindani mkubwa uliokuwepo kwa vyama vya siasa na jinsi kampeni zilivyoendeshwa.Uchaguzi kwa Tanzania bara naweza kusema ulifanyika vizuri pamoja na kasoro za hapa na pale kujitokeza lakini kwa Tanzania visiwani yaani Zanzibar zoezi la uchaguzi halikumalizika vizuri kwa  maana ya matokeo ya uchaguzi kufutwa.
Uchaguzi huo ulifutwa kwa kile kinachodaiwa kuwa uchaguzi ulikuwa na kasoro nyingi ambazo zilipelekea chombo chenye mamalaka yaani tume ya uchaguzi Zanzibar( ZEC) kupitia mwenyekiti wake kutangaza kufutwa kwa uchaguzi kwa sababu kuu niliyoileza hapo awali.Hali hiyo imepelekea kile kinachoitwa mkwamo wa kisiasa( Political impasse).Mkwamo huo wa kisiasa umeibua maswali mengi kwa watu mbalimbali na taasisi mbali mbali,kwa mujibu wa waangalizi wa ndani na nje wanasema zoezi lilienda vizuri hakuna kasoro zilizojitokeza kama inavyodaiwa na tume,wapo wengine wanauliza uhalali wa tume kwa maana ya tume kuwa zinajitokezaje kasoro kubwa zinazopelekea mpaka matokeo yote ya ya uchaguzi kufutwa, je tume haikuwa imejiandaa kuhakikisha zoezi linafanyika kwa weredi? Na wengine wanadai kitendo cha mwenyekiti kufuta matokeo bila kamati kukaa ni kinyume cha sheria kwa mujibu wa sheria ilivyo/inavoelekeza.
Hatuwezi kupuuza wasiwasi wa watu hao walionao juu ya kilichotokea Zanzibar.Kama  wakaguzi wa ndani na nje walijiridhisha na kuweza kutoa taarifa juu ya zoezi la uchaguzi kwenda vizuri,kwa nini tume ya uchaguzi iliamua kufuta matokeo ya uchaguzi huo?, je tume imeamua kufanya hivyo kwa maslahi ya nani?,mimi siamini kama matokeo yote yanaweza kuwa na kasoro wakati kuna watu maalum walikuwepo wakisimamia zoezi hilo kuhakikisha linafanyika vizuri. Kama tume imeamua kuchukua uamzi huo kwa maslahi ya watu wachache au chama,itambue kufanya hivyo ni kinyume na demokrasia na nikinyume na katiba,kama tuliamua kuwa nchi ya kidemokrasia na kuruhusu mfumo wa vyama vingi basi hatuna budi kukubaliana na matokeo ya mfumo huo.
Afrika imekuwa na changamoto kubwa hasa linapokuja suala la demokrasia na mfumo wa vyama vingi,vyama tawala vimekuwa vikitumia nguvu dora  kufunja sheria  na kukiuka katiba hasa vinapoonekana kuelekea kushindwa na vyama vya upinzani katika chaguzi,nafikiri hili ndilo limekuwa likipelekea hata matokeo ya uchaguzi kufutwa au kuchelewa kutangazwa kwa baadhi ya vituo vya uchaguzi.Nadhani  vyama tawala vinasahau kuwa wananchi ndiyo wenye nchi,hivyo wakiamua kuchagua chama wanachokiona kwao ni sahihi  hakuna sababu ya kutumia nguvu dora na ukiukwaji wa katiba kwa kupindisha sheria na kumweka mtu ambaye chama tawala kinamtaka,wananchi wameamua hivyo lazima tuheshimu maamuzi yao.Kama wazanzibari wameamua kumchagua wanayemtaka basi tuheshimu maamuzi yao na hiyo ndiyo demokrasia ya kweli.
Baada ya matokeo ya uchaguzi kufutwa ,tume hivi karibuni ilitangaza tarehe ya uchaguzi kurudiwa yaani tarehe 20 Machi,2016.Sikuona sababu ya msingi ya uchaguzi kurudiwa,huu mkwamo wa kisiasa ungeweza kutatuliwa kwa mazungumzo ya pande mbili kufanyika yaani CCM na CUF.Nikinukuu maneno ya Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi hivi majuzi katika sherehe za maadhimisho ya Chama cha Mapinduzi kutimiza miaka 39,”Alisema hakupenda uchaguzi urudiwe”.Nafikiri hiyo ingekuwa fursa  ya pande mbili yaaani CCM na CUF  kutanguliza maslahi ya taifa na mazungumzo kufanyika na hatimaye kufikia muafaka na matokeo kutangazwa.Kurudia  uchaguzi kwanza ni gharama na inaweza kupelekea wazanzibari kutokwa na imani na tume ya uchaguzi na mwisho inaweza kuleta uadui kwa vyama na serikali hasa kwa wananchi kuichukia serikali iliyopo na kuona hakuna sababu ya wao kushiriki katika chaguzi mbalimbali kwa sababu tume haiaminiki tena.
Mimi naamini, endapo Chama Cha Mapinduzi kikiamua kutanguliza maslahi ya taifa mbele basi  suluhu inaweza  kupatikana kwa urahisi,naamini mpaka sasa Chama Cha wananchi CUF kimeonesha ukomavu kwa kutaka suluhu iwepo.Hivyo fursa hiyo itumike vizuri kwa maslahi ya Zanzibar na Jamhuri ya muungano kwa ujumla .
Chagulani,Shabiru
10/2/2016